Kama 
tunavyofahamu, nchi yetu ina aina mbalimbali za nyoka ambao pindi 
wakimuuma mtu huleta madhara mbalimbali ya kiafya. Aidha tunafahamu 
kwamba tatizo hili lipo zaidi katika maeneo ya vijijini ambako uwezo wa 
wananchi kumudu gharama za matibabu ni mdogo.
Dawa za kutibu 
sumu ya nyoka huagizwa kutoka nje ya nchi. Dawa hizo siyo tu 
hazipatikani kwa urahisi, bali pia zinapatikana kwa gharama kubwa. Bei 
ya kununulia dawa hizi ni kati ya dola za kimarekani 55 hadi 85 (yaani 
shilingi za kiTanzania 118,250 hadi 182,750) kwa kichupa kidogo (vial) 
kimoja. Kichupa hicho huweza kutumika kwa wagonjwa wanne, lakini mara tu
 baada ya kufunguliwa dawa hiyo huwa haifai tena kutumika ndani ya mwezi
 mmoja tu.
Pamoja na 
changamoto hizo, Serikali kupitia MSD kila mwaka huagiza dawa hizi kwa 
ajili ya mahitaji hayo ya kutibu wagonjwa walioumwa na nyoka, ambapo bei
 ya kuinunua kutoka MSD ni TZS 200,000/= kwa kichupa kimoja. Hospitali 
zetu mbalimbali zimekuwa zikiagiza dawa hizi kutoka MSD na kwa washitiri
 wengine kwa bei hii au zaidi na kuwatibu waathirika wanaohitaji dawa za
 sumu za nyoka mara zinapohitajika. 

Napenda 
kuwakumbusha kwamba kwa mujibu wa Sera ya Afya ya mwaka 2007, huduma za 
tiba hutolewa bure kwa makundi maalum, au kwa kuchangiwa kwa sehemu ya 
gharama, au kwa kupitia mfumo wa Bima mbalimbali za Afya kama vile CHF. 
Kwa wale wasio na uwezo na wanaothibitishwa kuwa hawana uwezo, utaratibu
 wa msamaha hutumika.
Katika 
kuhakikisha kwamba wananchi wanaohitaji dawa ya  sumu ya nyoka 
wanahudumiwa ipasavyo, Mhe. Ummy Mwalimu, Waziri wa Afya, Maendeleo ya 
Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto anatoa maelekezo yafuatayo:-
Waganga Wakuu 
wa Mikoa na Viongozi wa Hospitali zote nchini wahakikishe kuwa Hospitali
 zote za umma zinaingiza dawa hii katika dawa za dharura ili iweze 
kununuliwa kama dawa zingine za dharura kupitia kifungu cha fedha za 
dawa za dharura.  
Kwa wagonjwa 
ambao watakuwa na Bima ya Afya, basi gharama za matibabu hayo zitalipwa 
kwa kupitia utaratibu huo wa Bima. Wananchi wanahimizwa kujiunga na Bima
 za Afya (CHF/NHIF) ili kupata unafuu wa matibabu haya na mengine. Mfano
 CHF - gharama ya kujiunga katika Halmashauri mbalimbali kwa kaya ni 
kati ya shilingi 5,000/= hadi shilingi 30,000/= kwa mwaka.
Kwa wagonjwa 
ambao watakuwa hawana Bima ya Afya, hao watatakiwa kuchangia gharama 
hiyo kwa nusu ya bei ya gharama ya dawa hizi au kwa kiwango kingine 
kitakachoamuliwa na Mganga Mkuu wa Serikali kadri itavyohitajika. Hii ni
 kutokana na ukweli kwamba kung'atwa na nyoka ni ajali na wananchi wengi
 wanaopatwa na ajali hii wapo maeneo ya vijijini ambao kimsingi uwezo 
wao wa kumudu gharama hizi kubwa za matibabu ya dawa ya sumu ya nyoka ni
 mdogo.
Wagonjwa 
watakaothibitika kuwa hawana fedha za kuchangia gharama hiyo, basi 
hospitali husika kwa kupitia mpango wa msamaha wa kulipia huduma za afya
 wahakikishe kwamba wanampatia mgonjwa huduma hizo kwa utaratibu wa 
msamaha wa gharama hizo.
Aidha, kwa kuwa
 nchi yetu ni kubwa na ina nyoka wengi, Mhe Waziri wa Afya anawaagiza 
Waganga Wakuu wa Mikoa na Halmashauri zote nchini kupitia kwa uangalifu 
takwimu za wagonjwa walioumwa na nyoka katika kipindi cha kuanzia mwaka 
2013 hadi 2016 na kuziwasilisha Wizarani kabla  ya tarehe 31 Januari 
2017 ili  kupata takwimu za mahitaji halisi ya dawa ya sumu ya nyoka 
nchini. Hii itasaidia  kuboresha upangaji, uagizaji na upatikanaji wa 
dawa hizo nchini. 
Vile vile, 
Waziri wa Afya ameiagiza Bohari ya Dawa (MSD)  kuweka utaratibu wa 
haraka wa kununua dawa hizo moja kwa moja kutoka kwa wazalishaji ili 
kupata unafuu wa bei.
 RSS Feed
 Twitter

10:48 AM
MZM

 Posted in 
0 comments:
Post a Comment