Serikali imerejesha mafunzo ya madereva kila baada ya miaka mitatu wakati wa kumalizika kwa muda wa leseni zao, huku ikifafanua kuwa elimu watakayoipata ina umuhimu katika kazi zao, kutokana na mabadiliko mbalimbali yanayotokea katika sekta hiyo.
Naibu
 Waziri wa Kazi na Ajira, Makongoro Mahanga, alitangaza uamuzi huo wa 
Serikali jana katika mkutano kati yake na viongozi wa madereva wa mabasi
 nchini.
Mkutano
 huo umefanyika kama ilivyoahidiwa na Waziri wa Kazi na Ajira, Gaudensia
 Kabaka, wakati alipokuwa akijitahidi kumaliza mgomo wa madereva 
uliofanyika Aprili 10 mwaka huu, wakati walipokuwa wakipinga pamoja na 
mambo mengine, sharti la kwenda shule ili kupata leseni mpya.
Madereva
 hao walitaka Serikali ifanyie marekebisho Sheria ya Usalama Barabarani,
 kwa kuondoa kipengele kinachowataka madereva kwenda Chuo cha Taifa cha 
Usafirishaji (NIT) kwa mafunzo ya muda mfupi kila wakati leseni zao 
zinapoisha, ili kupata sifa ya kupata leseni nyingine.
Sababu
 ya kupinga kupata mafunzo, ilidaiwa kuwa utaratibu huo uliotangazwa 
Machi 30, mwaka huu, ulianzishwa bila kushirikisha madereva katika 
kuuandaa.
Pia
 walipinga kutakiwa kujilipia gharama za shule hiyo ambazo walidai ni Sh
 560,000 kwa magari ya kawaida na Sh 200,000 kwa magari ya abiria.
Sababu
 nyingine iliyochangia wapinge shule hiyo, walidai ni kukosekana kwa 
mikataba ya ajira, inayoweza kuwahakikishia kulindwa kwa kazi zao hadi 
wanapomaliza mafunzo.
Madai
 mengine yaliyokuwa nje ya shule hiyo, madereva hao walitaka kuondolewa 
kwa faini ya Sh 300,000 kwa kila kosa la barabarani na kuitaka Mamlaka 
ya Udhibiti wa Usafiri wa Majini na Nchikavu (Sumatra), kuhakiki 
uhalisia wa dereva anayeandikishwa na mmiliki wa chombo husika.
Majibu
 ya Serikali Mahanga aliyekuwa Mwenyekiti wa kikao hicho, alisoma tamko 
la Serikali lililoeleza kuwa pamoja na kurejesha mafunzo hayo, 
utekelezaji wake hautafanyika mara moja kwa kuwa Kanuni zake 
hazijakamilika.
“Tangazo
 hili (la kwenda shule) limetolewa kwa kuzingatia umuhimu wa mafunzo 
kazini kwa wafanyakazi na madereva kama ilivyo kwa wafanyakazi wengine,”
 alisema Mahanga.
Alisisitiza
 kuwa baada ya miaka mitatu ya leseni, dereva atatakiwa kupata mafunzo 
mafupi, ambayo ni kati ya siku tatu hadi saba na atakayegharimia mafunzo
 hayo ni mwajiri, si mfanyakazi na ni katika chuo chochote 
kinachotambulika.
Akifafanua,
 Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Ndani, Mwamini Malemi aliyekuwepo 
katika mkutano huo, alisema mitaala ya mafunzo hayo bado inaandaliwa, 
hivyo si rahisi Kanuni hiyo kuanza kutekelezwa mwaka huu hata kama 
zitakamilika.
Kuhusu
 mikataba ya ajira ambayo ililalamikiwa mno na madereva wakati wa mgomo,
 Mahanga alisema Serikali itapitia upya mikataba hiyo ili kuhakikisha 
mambo yote muhimu yanazingatiwa.
Akiongezea
 hoja katika suala la mikataba, Malemi alisema ni lazima mikataba iwe 
imekamilika kabla ya kuanza kutumika kwa kanuni ya kwenda shule, ili 
ioneshe wajibu wa mwajiri katika kumsomesha mfanyakazi.
Kuhusu
 kauli iliyotolewa na Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, 
Suleiman Kova ya kuondoa tochi za kupima mwendo kasi barabarani, Mahanga
 alisema matumizi ya tochi zinazotumika kupima mwendo kasi na ratiba ni 
sehemu ya utekelezaji wa Sheria za Usalama Barabarani.
Hoja
 nyingine Katika kikao hicho mbali na hoja zilizosababisha mgomo, 
kulikuwa na hoja nyingine zilizowasilishwa, ikiwemo changamoto ya 
madereva kupata maelekezo yanayokinzana kutoka Jeshi la Polisi na 
Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Nchikavu na Majini (Sumatra), kuhusu 
ratiba ya kuondoka wanakotoka na kuwasili wanakokwenda.
Akitoa
 majibu ya Serikali, Mahanga alisema amepokea hoja hiyo na ataifanya 
utafiti wa kina. Katika hoja ya kuwataka waajiri kuongeza posho za kazi,
 Mahanga alisema Serikali haiwezi kupanga posho za madereva katika kikao
 hicho, kwasababu kila mwajiri ana uwezo wake kulingana na safari za 
gari yake.
Hata
 hivyo, aliahidi kufanyika utafiti suala hilo katika nchi nyingine, ili 
aone namna ambavyo madereva wengine wamekuwa wakilipwa posho.
Serikali
 pia imeahidi kuimarisha ukaguzi sehemu za kazi kwa kushirikiana na 
Sumatra, utakaohusu wamiliki wa magari na kuhuisha mfumo wa kumbukumbu, 
utakaoonesha kila gari na dereva wake halisi na kuweka vitambulisho vya 
dereva katika kila gari analoendesha.
Mahanga
 alisema Serikali pia itaweka utaratibu mpya ambapo dereva mwenyewe 
atajiwekea bima ya ajali itakayoanzishwa na kujiunga na vyama vya 
wafanyakazi, ili watetee mikataba yao ili iweke pia maswala ya bima 
hizo.
Alisema pia Serikali imeanzisha Mfuko wa Fidia ya Wafanyakazi, ambao utaanza hivi karibuni, ambao mwajiri atawajibika kuchangia.
Chama cha Wafanyakazi 
Kuhusu
 chama cha wafanyakazi, Mahanga alisema Serikali imepokea pendekezo la 
kusaidia madereva kuunda chama cha wafanyakazi chenye nguvu, ambapo 
alisema kumbukumbu zinaonesha madereva wana vyama vilivyosajiliwa kwa 
Msajili wa Vyama vya Wafanyakazi na Waajiri.
Alitaja
 vyama hivyo kuwa ni Umoja wa Wafanyakazi wa Mawasiliano na Usafiri 
Tanzania (COTWU), kilichosajiliwa mwaka 2000 na Chama cha Wafanyakazi 
cha Usafiri wa Barabara (TARWORTU) kilichosajiliwa mwaka 2013.
“Katika
 kushughulikia changamoto za wafanyakazi na mwajiri wote mnategemeana, 
jambo mtakalofanya ni kuanzisha majadiliano kupitia vyama vya 
wafanyakazi lakini kwanza muwe ndani ya vyama,” alisema Mahanga.
Wanung’unika 
Baada
 ya kusomwa kwa tamko hilo la Serikali, Katibu Mkuu wa Vyama vya 
Madereva Tanzania, Mwanarashidi Salehe, alisema mafunzo wanayotakiwa 
kuchukua hayana tija yoyote, kwa kuwa wakufunzi ni wa kizamani na pia 
magari yanayotumika ni ya kizamani, ambayo hayaongezi chochote katika 
kazi yao.
“Kwanza
 hakuna kipya katika mafunzo hayo, mimi nimehudhuria mara mbili....pili 
katika kikao hiki tulitarajia tutakutana na wamiliki wa magari ambao 
ndio waajiri wetu ili waseme waliyonayo juu yetu na sisi tuseme yetu 
tujadiliane na kupata majibu,” alisema Salehe.
Mwenyekiti
 wa chama hicho, Clement Masanja alisema mikataba waliyonayo madereva ni
 dhaifu mno, haioneshi mambo ambayo dereva atanufaika nayo.
“Tulitarajia
 katika kikao hiki tutatoka na majibu ya posho za madereva, ili dereva 
ajue atalipwa kiasi gani kwa safari za ndani na nje ya nchi kwa sababu 
anavyolipwa ni manyanyaso matupu,” alisema Masanja.
 RSS Feed
 Twitter

6:29 AM
MZM


0 comments:
Post a Comment