Saudi Arabia imesema majeshi yake yamewauwa na waasi wa Yemen waliofanya
 shambulizi lao la kwanza kubwa dhidi ya nchi hiyo tangu kuanza mwezi 
uliopita mashambulizi ya angani yanayoongozwa na Saudia
Wizara ya ulinzi ya Saudi Arabia imesema wanajeshi wake watatu pia 
waliuawa katika mapambano hayo baada ya waasi wa Houthi kuvilenga vituo 
vyao vya uangalizi, wakati jeshi lake likijaribu kuzuia shambulizi hilo.
Kumekuwa na makabiliano hapo kabla lakini hii ni mara ya kwanza ambapo 
jeshi la Saudi Arabia limeripoti kuhusu shambulizi kamili la waasi wa 
Houthi katika mipaka yake. Katika mji mkuu Sanaa, mashambulizi mapya ya 
kutokea angani yanayoongozwa na Saudia yamefanywa katika uwanja wa ndege
 ikiwa ni siku chache tu baada ya ndege za kivita kuilipua njia ya ndege
 katika uwanja huo ili kuzuia ndege moja ya Iran kutua.
Wakati huo huo, mawaziri wa mataifa ya Ghuba hapo jana walipinga 
pendekezo la kuandaa mazungumzo katika nchi isiyounga mkono upande 
wowote katika mzozo wa kisiasa nchini Yemen, wakati ripoti ya watalaamu 
ikisema kuwa Iran imekuwa ikiwapa silaha waasi wa Houthi tangu mwaka wa 
2009.
Umoja wa Mataifa unajaribu kumaliza operesheni ya angani iliyodumu wiki 
kadhaa, na kuzirejesha pande zote mbili katika meza ya mazungumzo. Baada
 ya mkutano wa mjini Riyadh, mawaziri wa nchi za Ghuba walisisitiza kuwa
 mazungumzo baina ya makundi hasimu ya kisiasa nchini Yemen yaandaliwe 
nchini Saudi Arabia, ambayo inaongoza muungano wan chi za Kiarabu dhidi 
ya waasi wa Kishia tangu Machi.
Iran inapendekeza kuandaa mazungumzo ya Umoja wa Mataifa ili kumaliza 
vita nchini Yemen katika taifa lisiloegemea upande wowote, ambalo 
haliwakilishwi katika muungano unaoongozwa na Saudia.
Baraza la Ushirikiano wa Ghuba lenye nchi sita wanachama limesisitiza 
kuunga mkono juhudi kali zinazofanywa na serikali halali ya Yemen za 
kuandaa mkutano chini ya mwamvuli wa Baraza hilo mjini Riyadh.
Katibu Mkuu wa Baraza hilo Abdullatif al-Zyani amesema mkutano huo 
utahudhuriwa na “pande zote za Yemen na zinazounga mkono uhalali na 
usalama na uimara wa Yemen”.
Mkutano wa jana wa nchi za Ghuba ambazo ni Bahrain, Kuwait, Oman, Qatar 
na Umoja wa Falme za Kiarabu, ulilenga kuweka msingi wa mkutano mkuu wa 
viongozi wa Baraza hilo utakaoandaliwa Jumanne wiki ijayo, na ambao pia 
utahudhuriwa na Rais wa Ufaransa Francois Hollande.
Mgogoro huo umeongeza mivutano katika kanda hilo. Iran inayotuhumiwa kwa
 kuwapa silaha waasi wa Houthi, imesema meli zake mbili zilizotumwa 
katika Ghuba ya Aden zimefika mlango wa Bab al-Mandab, njia muhimu ya 
bahari baina ya Yemen na Djibouti. Iran inasisitiza kuwa meli zake hizo 
hazitafika katika mipaka ya bahari ya nchi nyingine.
 RSS Feed
 Twitter

9:26 AM
MZM

0 comments:
Post a Comment